Tuesday, 1 October 2013

KIBURI CHAMPONZA: MOYES AKATAA USHAURI WA FERGUSON

MANCHESTER, ENGLAND
NI kiburi! Ni jeuri. David Moyes kumbe alikataa ushauri wa kocha aliyepita wa Manchester United, Sir Alex Ferguson, aliyemtaka aendelee kuwa na watu wake wa benchi la ufundi, lakini yeye akawatimua na kuleta watu wake.
Hali ya Moyes ni mbaya Old Trafford baada ya timu hiyo kupata pointi saba katika mechi sita na kocha wa zamani wa makipa wa Manchester United chini ya utawala wa Ferguson, Eric Steele, ametia chumvi kidonda baada ya kusema kuwa Moyes ni mbishi.
Steele alionyeshwa mlango wa kutokea na Moyes pamoja na wasaidizi wengine wa zamani wa Ferguson, Mike Phelan na kocha wa timu ya kwanza, Rene Meulensteen.
Badala yake, aliamua kuwaleta Chris Woods, Steve Round na Jimmy Lumsden ambao alikuwa nao Everton huku pia akimteua beki wa zamani wa United na Everton, Phil Neville kuwa mmoja wa wasaidizi wake.
“Aliongea na mimi, Mick na Rene. Nilimwambia kwamba nadhani ulikuwa uamuzi wa kishujaa. Alisikiliza ushauri wa Ferguson, lakini akataka awe mtu mwenye uamuzi wake mwenyewe,” alisema Steele.
Steele aliwasili Man United mwaka 2008 baada ya kufanya kazi na
Manchester City kabla ya hapo. Anasifika kwa kumgeuza David De Gea kuwa mmoja kati ya makipa bora duniani baada ya kuanza Ligi Kuu England hovyo.
Anasema kwamba anaheshimu uamuzi wa Moyes wa kuachana na wao, lakini akaongeza kwamba haukuwa uamuzi mzuri kwa maendeleo ya klabu.
“Sikutaka kuondoka. Nilijua kwamba David alikuwa anakuja na nikawa najiuliza angekuja na nani. Simlaumu kwa alichokifanya, nimekuwa katika soka kwa muda mrefu sana, lakini inashangaza kidogo,” alisema.
“Umekutana na timu ambayo ilikuwa na msimu mzuri na imeshinda ligi. David De Gea alikuwa na msimu bora. Inaleta maana kama hautaki kuendelea kufanya kazi na watu waliokuwapo. Hata hivyo hilo lipo nje ya uwezo wangu.”
Kipigo cha mabao 2-1 cha Man United kutoka kwa West Brom Jumamosi katika uwanja wao wa nyumbani, Old Trafford, kinaiacha United  ikiwa na pointi saba katika nafasi ya 12 ikiwa ni pointi nane nyuma ya vinara Arsenal.
 



No comments:

Post a Comment