Thursday, 31 October 2013

RAIS WA FIFA SEPP BLATTER AOMBA RADHI KWA CHRISTIANO RONALDO NA KLABU YA REAL MADRID.

Rais WA FIFA Sepp Blatter amelazimika kuomba radhi kwa maneno aliyoyatoa dhidi ya Cristiano Ronaldo wakati alipokuwa anazungumza na wanafunzi wa chuo cha Oxford nchini Uingereza . Blatter alitoa maneno yalioonekana kama ya dhihaka dhidi ya Cristiano Ronaldo wakati alipokuwa anamzungumzia akijaribu kumfananisha na mchezaji wa Barcelona Lionel Messi
.
Blatter alimzungumzia Messi huku akimtaja kama “Mtoto mtiifu ambaye anamvutia mtu yoyote ambaye ni mzazi kumpenda” , ana tabia nzuri ,ni mpole na hana makuu,zaidi ya yote ni mchezaji ambaye ana uwezo wa kipekee unaotokana na kipaji halisi kilichopo miguuni mwake ambapo akicheza mpira uwanjani anaonekana kama anacheza muziki.
Blatter hakuishia hapo na akahamia kwa Ronaldo ambapo alimtaja kama mchezaji ambaye huwaamrisha wenzie uwanjani kama inavyokuwa vitani kwa kamanda anayewaamrisha wenzie (Blatter alisema hayo huku akiigiza mikogo au swaga za Ronaldo anapokuwa uwanjani) , Blatter aliendelea kusema kuwa Ronaldo anatumia fedha nyingi kwa ajili ya masuala ya urembo hasa nywele zake tofauti na Messi ambaye masuala hayo hayamsumbui kichwani mwake . Blatter aligongelea msumari wa mwisho kwa kusema kuwa kwake Messi ndio chaguo la kwanza .
Hii ni kauli ambayo Ronaldo hakuipenda na alijibu mapigo kwenye ukurasa wake wa Facebook ambapo alituma ujumbe uliokuwa unaonekana kama unampiga dongo Blatter ambapo kwenye ujumbe huo alimalizia kwa kusema kuwa “Namtakia Blatter afya njema na maisha marefu ili aweze kuwashuhudia wachezaji anaowapenda na timu anazopenda zikipata mafanikio.
RONALDO FB
Blatter alijirudi baadaye na kuomba radhi kwa kauli aliyoitoa akisema kuwa haikueleweka katika muktadha sahihi na halikuwa lengo lake kumkosea heshima Ronaldo na klabu ya Real Madrid.


No comments:

Post a Comment