Kituo hicho pia kimelaani kauli za viongozi wa
Bunge maalumu la Katiba na Serikali za kutaka kuzuiwa mijadala ya Katiba
kufanywa nje ya Bunge hilo na vyombo vya habari.
Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dk Hellen
Kijo-Bisimba aliwaambia waandishi wa habari jijini hapa jana kuwa hakuna
haja ya kufanya haraka katika kupata Katiba Mpya ambayo haitakuwa na
maridhiano na kwamba kulazimisha kuipata ni kutafuta machafuko.
“Tunapendekeza Bunge la Katiba kusitisha mijadala
ya sura zilizosalia na kufanya kila liwezekanalo kumaliza mgogoro kati
yao ili majadiliano yakiendelea kuwe na uhakika wa kufikia kupiga kura
na mapendekezo mapya yawe na uhalali wa kisheria na kisiasa.
“Tuna uzoefu wa nchi nyingi zilizolazimisha
masuala kama haya baadaye yakaleta mtafaruku. Watu wasiseme tu kuwa ni
watu wachache waliosusia Bunge hapana… wale watu wana wafuasi wengi
wanaowafuata ambao wanaweza kuleta balaa,” alisema Dk Bisimba.
Alisema wajumbe wote wanaoendelea na vikao katika
Bunge Maalumu la Katiba hawana uhalali kuendelea kujadili rasimu hiyo
kwa kuwa umoja unaowatambulisha kama wajumbe wa kuandaa katiba ya
Tanzania ulishavunjika.
Bunge maalumu linaendelea na vikao vyake kujadili
sura 15 za Rasimu ya Katiba, baada ya kumaliza sura ya kwanza na sita
katika awamu ya kwanza, safari hii bila kuwa na wajumbe wa kutoka Umoja
wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Wajumbe wa umoja huo unaoundwa na vyama vya
Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi walitoka bungeni Aprili 16, mwaka huu
wakipinga mwenendo baadhi ya wajumbe kujadili masuala yaliyo nje ya
rasimu ya pili kama yalivyopendekezwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba
iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba.
Dk Bisimba alibainisha kuwa hakuna haja ya kukata
tamaa kutafuta maridhiano na kuongeza kuwa ili kupata mwafaka,
wanahitajika wasuluhishi wasiofungamana na upande wowote unaokinzana.
Kuhusu kauli za kuzuia mijadala ya Katiba nje ya
Bunge pamoja na kuwazuia waliokuwa wajumbe wa Katiba kutoa maoni yao, Dk
Bisimba alisema hatua hiyo ikitekelezwa itakiuka misingi ya demokrasia
na utawala wa sheria na kuminya uhuru wa vyombo vya habari na haki za
binadamu kama zilivyobainishwa katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ya mwaka 1977.
Alisema pendekezo lililotolewa hivi karibuni na
Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta la kutaka Serikali kupiga
marufuku vyombo vya habari kurusha matangazo ya mijadala ya katiba
pamoja na agizo la Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Rehema Nchimbi kuzuia
mijadala hiyo katika mkoa wake ni kinyume cha Ibara za 18 na 21 ya
Katiba iliyopo.
“Tabia hii ya kuwafunga midomo watoa habari na
kuwafumba macho wananchi ili wasiweze kushiriki kikamilifu katika
kuandika Katiba yao, haikubaliki kamwe na ni kinyume cha misingi ya
demokrasia,” alisema Dk Bisimba.
No comments:
Post a Comment