Daalal akimsindikiza Aveva kurejesha fomu leo |
Monday, 12 May 2014
DALALI AMPA MAAGIZO MAZITO AVEVA NA MPIRA JUU
ALIYEWAHI
kuwa Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Hassan Daalal amemtaka mgombea Urais
wa klabu hiyo, Evans Aveva avunje makundi saba yanayoigawa klabu hiyo
kwa sasa, iwapo atafanikiwa kuingia madarakani.
Ameyataja
makundi hayo kuwa ni Simba Ushindi, Robialac Friends, Simba Chai, Simba
Futari, Tia Mchuzi Kwangu Pakavu na Simba Poa ambayo ni ile inayofurahi
hata timu yao ikifungwa.
Daalal
leo amemsindikiza Aveva kurejesha fomu ambayo aliichukua jana kuwania
cheo hicho katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi
ujao.
Dalali
amesema kuwa alikuwa na nia ya kuwania cheo hicho lakini baada ya kuona
Aveva amechukua fomu aliamua kuacha dhamira yake na kuwataka wanachama
wa Simba kumchagua mgombea huyo kwa sababu ni mtu mwadilifu, mwaminifu,
mwenye upendo na asiye na ubaguzi.
Alisema
kwamba anaamini Aveva akichaguliwa atahakikisha anamaliza makundi
yaliyopo ndani ya klabu yao, ataleta umoja na kuendeleza mazuri ya ndani
ya uwanja ambayo ni kupata pointi tatu.
"Nilipoondoka
mwaka 2010 niliondoka na mpira wangu, sasa nakukabidhi ili uhakikishe
pointi tatu zinapatikana, na ninaamini atawarudisha wazee ambao miaka
minne iliyopita walifukuzwa, nyumba bila ya wazee haiendi," alisema
Dalali.
Katibu
Msaidizi wa Kamati ya Uchaguzi, Khalid Kamguna, alisema kuwa bado
anatoa wito kwa wagombea kujitokeza kuchukua fomu kuwania nafasi hizo
saba zilizotangazwa ili waweze kuitumikia klabu hiyo.
Kamguna
aliwataja wagombea wengine ambao walichukua fomu jana mbali ya Wambura
kuwa ni pamoja na Meddy Milanzi, Collin Frisch, Chano Hassan, Khamis
Mkoma, Salim Jazaa, Emmanuel Kazimoto, Juma Abbas (Pinto) na Amina Poyo
ambaye ndiye mwanamke pekee ambaye amejitokeza katika uchaguzi huo
nafasi ya Ujumbe wa Kamati ya Utendaji.
Aliwataja
wagombea waliorejea kuwa ni Iddi Kajuna, Ramson Rutiginga, Said Tully,
Suleiman Dewji wanaowania Ujumbe wa Kamati ya Utendaji na Andrew Tupa
anayegombea cheo cha Urais wa Simba.
Alisema kuwa mwisho wa zoezi hilo la kuchukua na kurejesha fomu ni kesho Jumatano saa 10 kamili jioni.
Labels:
sports
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
No comments:
Post a Comment